Simba imepokwa pointi za Kagera Sugar

Shirikisho la Soka la Tanzania (TFF) limetangaza kuipoka Simba pointi tatu na mabao matatu ambazo ilipewa kutokana na mchezo wao dhidi ya Kagera Sugar.


 Wiki mbili zilizopita Simba ilipoteza mchezo dhidi ya Kagera kwa kufungwa mabao 2-1 kwenye Uwanja wa Kaitaba mkoani Kagera katika Ligi Kuu ya Bara lakini baadaye ilikata rufaa ikipinga Kagera kumtumia mchezaji Mohamed Fakhi ikidai alikuwa na kadi tatu za njano, ndipo ikapewa ushindi huo kupitia Kamati ya Saa 72.

 Maamuuzi haya yanakuja baada Kagera Sugar kuomba kufanya marejeo ya hukumu yao ya kupokwa pointi tatu na kamati ya saa 72 kwa madai ya kumchezesha Mohamed Fakhi mwenye kadi tatu za njano, ndio Katibu wa TFF akaitisha kikao cha kamati ya katiba, sheria na hadhi za wachezaji kupitia marejeo (review) ya hukumu hiyo.

KAMATI ya Katiba, Sheria na Hadhi za wachezaji imetengua maamuzi ya kamati ya Usimamizi na mashindano (kamati ya saa 72) kwa kuipoka Simba pointi tatu na mabao walizopewa na kamati ya saa 72 kwa madai ya kumchezesha Mohamed Fakhi mwenye kadi tatu za njano.

Akizungumza na waandishi wa habari juu ya uamuzi huo, Katibu Mkuu wa TFF, Selestine Mwesigwa amesema kuwa kuna sababu kadhaa zimechangia kuchukuliwa kwa maamuzi hayo ambapo alizitaja kuwa ni:
“Malalamiko ya Simba hayakuwasilishwa kwa wakati muafaka tangu mchezo ulipochezwa, malalamiko yao hayakuwa katika njia ya maandishi, rufaa ya Simba haikulipiwa ada, kikao cha Kamati ya Saa 72 kilikosa uhalali kutokana na kuwashirikisha watu ambao hawana uhalali wa kuwa kwenye kikao.

 “Kutokana na sababu hizo kamati imeamua kutengua maamuzi yaliyochukuliwa na Kamati ya Saa 72 na kurejesha matokeo kama yalivyokuwa, pia kamati imemuagiza katibu mkuu wa TFF kuwapeleka baadhi ya wajumbe wa bodi ya ligi katika Kamati ya Maadili ya TFF kwa kosa la kwenda kinyume na kazi zao,” alisema Mwesigwa.

 Pia Mwesigwa amesema maamuzi yaliyofikiwa na kamati ya katiba, Sheria na hadhi za wachezaji ni ya Mwisho hayakatiwi rufaa sehemu yoyote.
Share:

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Social